Utafiti
huu uliochapishwa katika Jarida la Tiba la Kiharusi umesema kuwa, mada hiyo
hupatikana kwa asilimia 82 kwenye machungwa na juisi ya machungwa, na
hupatikana kwa asilimia 14 kwenye zabibu na juisi ya zabibu. Hata hivyo
watafiti hao wamesema kwamba, kwa wale wenye kusudio la kuongeza kiwango
kikubwa cha flavanones itawalazimu kula tunda
asili la chungwa kwa wingi na si
juisi za machungwa zinazotengenezwa kiwandani kutokana na kuwa na kiwango
kikubwa cha sukari katika juisi hizo. Flavanones hutoa kinga dhidi ya kiharusi
kutokana na kuongeza ufanisi wa mishipa ya damu kwenye ubongo na kutokana na
kuwa na uwezo wa kuzuia maambukizi mwilini.
Lakini ni vyema tukawa makini pia kuwa matokeo
ya utafiti huu yasiwafanye watu kuacha kula matunda ya aina nyingine pamoja na
mboga za majani kwani nayo yana faida kubwa katika mwili wa binadamu. Pia
tukumbuke kuwa, inawezekana kupunguza uwezekano wa kupata kiharusi kama mtu
atakula lishe bora iliyo na virutubisho vyote muhimu, kula matunda na mboga za
majani kwa wingi, kufanya mazoezi mara kwa mara, kupunguza kiwango chumvi
tunachokula, (kwani watu wenye asili ya Afrika wana kiashiria cha asili kinachojulikana
kama salt retention gene ambacho hufanya kiwango kidogo cha matumizi ya chumvi
mwilini kionekane kikubwa na hivyo kuongeza hatari ya kupata kiharusi),
kupunguza uzito, kupunguza kiwango cha matumizi ya mafuta katika chakula,
kulala masaa ya kutosha na kupunguza msongo wa mawazo.
